Tuesday, 19 August 2014

TAARIFA KAMILI YA HABARI YA RASI FM RADIO 103.7--DODOMA.... SOMA MTANDAONI

DODOMA                                                                    19.08.2014

Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM inakutana leo mchana mjini Dodoma chini ya mwenyekiti wake, Rais Jakaya Kikwete huku ikitarajiwa kufanya uamuzi mgumu wa mchakato wa Katiba.

Kikao hicho kinakutana kwa mara ya pili katika muda mfupi, baada ya hivi karibuni kukaa  jijini Dar es Salaam kikiwa na lengo la kujadili mchakato wa Katiba unaoendelea



Akizungumzia kikao hicho, mtaalamu wa sayansi ya siasa na utawala katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dokta Alexander Makulilo amesema jambo kubwa litakalojadiliwa katika kikao hicho ni kauli tofauti zilizotolewa na wananchi kuhusu mchakato wa kupata Katiba Mpya.

Duru za habari  zinadai kuwa kikao hicho kinaweza kupendekeza kuwashughulikia wanachama wake waliotoa kauli zinazopingana na msimamo wa chama hicho.
                                                   MWISHO.



KILIMANJARO                                                                 19.08.2014
Jamii imeshauriwa kuchukua tahadhari kwa kunawa mikono kabla na baada ya kula ili kuweza kujikinga na maambukizi ya magonjwa ya milipuko.
Ushauri huo umetolewa na Ofisa Afya Mratibu wa Kampeni ya Usafi wa Mazingira wa Halmashauri ya Wilaya ya Siha mkoani Kilimanjaro Bibi  Joyce Tarimo wakati akizungumza na wakuu wa Shule, waratibu elimu , wenyeviti wa bodi za shule, na wenyeviti wa viijiji iliyolenga utekelezaji wa mikakati ya taifa ya kampeni ya usafi iliyofanyika kwenye ukumbi wa kanisa katoliki wilayani Siha.
Awali akitoa mada katika Semina hiyo Afisa wa Kitengo cha Afya na Mazingira Wilayani siha Lidya Joseph amewataka viongozi kusaidia kuelimisha jamii namna ya kujikinga na Maradhi hayo.
Nae Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri hiyo Bwana Rashidi Kitambulio amewataka viongozi hao kuacha tabia ya kutoa maagizo badala yake watumie muda mwingi kuielimisha jamii madhara ya uchafu .
Hata hivyo  Bwana Kitambulio amesema Serikali imejipanga vyema kuhakikisha maradhi hayo hayasambai ,kwa kutoa elimu mbalimbali sambamba na kuendesha vipindi vya dharura kwa jamii ili kupunguza maradhi hayo.
                                                      MWISHO.


DAR  ES  SALAAM                                                       19.08.2014

Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam limetumia mabomu ya machozi kuwatawanya watu wenye ulemavu wa ngozi (albino), waliokuwa wakizuia gari la polisi lililokuwa limebeba mtuhumiwa wa kutishia kuua  Albino kwa maneno.

Tukio hilo limetokea jijini Dar es Salaam ambapo walemavu wa ngozi hao wamevamia gari hilo na kuwataka askari polisi wamshushe ndani ya gari mtuhumiwa huyo aliyetambulika kwa jina la Ombeni Michael, ili wafahamu alipokuwa  akipelekwa.

Vurugu hizo zilianza katika Mahakama ya Mwanzo Buguruni, ambapo walemavu hao walivamia wakati kesi dhidi ya mtuhumiwa huyo ikiendelea katika mahakama hiyo.

Baada ya kusikilizwa kwa kesi hiyo na dhamana kuwa wazi kwa mujibu wa sheria, watu hao wenye ulemavu waliamsha hasira ya kupinga kupewa dhamana kwa mtuhumiwa huyo.

Kesi hiyo iliahirishwa hadi Septemba 3, mwaka huu.

Aidha Mwekahazina wa Chama cha Albino Tanzania, Abdillah Omary, alilazimika kuandika barua mahakamani hapo kupinga hatua ya kupewa dhamana kwa mtuhumiwa huyo.

Kamanda wa Polisi Wilaya ya Ilala, Mary Nzuki, amethibitisha kutokea kwa vurugu hizo, huku akisema kuwa hali hiyo imechangiwa na mwili wa mwanamme mmoja aliyedhaniwa ni mlemavu wa ngozi kuokotwa amefariki dunia Tabata Kinyerezi mwishoni mwa wiki iliyopita.

                                                MWISHO.


DODOMA                                                              19.08.2014

Wakazi wanaopitiwa na mradi wa umeme wa vijijini (Rea) Mkoani Dodoma wamelalamika kufanyiwa vitendo vya utapeli vinavyofanywa na watu wanaofahamika kama vishoka.

Akizungumza na kituo hiki mmoja wa wakazi wa kijiji cha Makoja Wilayani Chamwino Bwana Matonya Msena amesema  vishoka hao wamekuwa wakipita  nyumba hadi nyumba na kuwatoza michango ya kusaidia kuwaunganishia umeme Kwa gharama ya shilingi laki moja hadi laki tatu wakati gharama halisi za kuunganisha nishati hiyo ni shilingi elfu thelatihini na mbili na mia tisa tu.

Amesema kutokana na tabia hiyo ambayo tayari wakazi wengi wameshatapeliwa fedha zao kwa vishoka hao,wameliomba shirika la Tanesco kutoa elimu kwa wananchi ili kuweza kuwatambua wahalifu hao.

Amesema elimu hiyo pia itaweza kusaidia hata kuwachukulia hatua za kisheria pindi watakapokamatwa hao vishoka ili kukomesha tabia hiyo.

Kwa upande wao Afisa masoko wa shirika la Tanesco Makao Makuu  Bibi Jennifer Mgendi na Mhandisi afya na usalama Tanesco Athanas Zawadi Wamesema mradi wa umeme vijijini Rea Mkoani Dodoma umeanza kutekelezwa kuanzia mwezi january mwaka 2014 na unatarajiwa kukamilika ifikapo june 2015, kwa gharama ya zaidi ya shilingi bilioni 54 huku wakazi wa vijiji vinavyopitiwa na mradi huo wakiwa na matarajio makubwa ya kujikwamua kiuchumi.
                                                    MWISHO.


NAIROBI                                                                            19.08.2014
Kampuni ya ujenzi ya China imesema imewaajiri wakenya wapatao 2,464 kwa ajili ya kazi ya mwanzo ya mradi wa kujenga reli unaotarajiwa kurahisisha usafirishaji wa bidhaa nchini humo.
Akizungumza mjini Nairobi baada ya kufanya mazungumzo na rais wa Kenya Uhuru Kenyatta,  mwenyekiti msaidizi wa kampuni ya ujenzi ya China, Bwana  Wen Gang, amesema kampuni yake itatoa ujuzi na kuwapeleka  watu wa Kenya ili kusaidia nchi katika utengenezaji wa vifaa vya mradi huo wa ujenzi.
 Amesema hadi mwishoni mwa mradi huo, zaidi ya wakenya 30,000 watakuwa wameajiriwa moja kwa moja na asilimia 40 ya kazi zitakwenda kwa makampuni ya Kenya.
Wakati wa mkutano huo rais Kenyatta amepongeza ahadi za kampuni hiyo za kushirikiana na wenyeji ili kusukuma mbele kiwanda cha utengenezaji chuma nchini humo.
Reli hiyo inalenga kutoa ufanisi na gharama nafuu za usafiri wa reli kwa mizigo na abiria.
                                                  MWISHO.


WASHINGTON                                                        19.08.2014
Rais wa Marekani Barack Obama amesema majeshi ya Iraq na yale ya Kikurd yamepiga hatua kubwa kulitwaa tena bwawa muhimu la Mosul kutoka kwa wapiganaji wa kiislamu kaskazini mwa Iraq.

Amesema wamethibitisha kwamba wanauwezo wa kufanya kazi kwa pamoja na wataendelea kuungwa mkono na majeshi ya Marekani, ambayo tayari yamefanya mashambulio Zaidi ya anga katika eneo linalokaliwa na wapiganaji wa kiislamu.

Ripoti zinasema kuwa mapambano katika juhudi za kudhibiti maeneo yanayozunguka bwawa hilo yanaendelea.

Katika hatua nyingine kundi la himaya ya kiislamu linalofanya mashambulizi dhidi ya Wakurd limekanusha kwamba wapiganaji wake wamepoteza udhibiti wa bwawa hilo.

Wakati huohuo kiongozi wa kanisa katoliki duniani papa Francis amesema jumuiya ya kimataifa itakuwa na haki katika kuchukua hatua dhidi ya wanamgambo hao.Amesema ni halali kuzuia kile alichokiita dhuluma ya kichokozi.

                                                       MWISHO.

 SIOL                                                                        19.08.2014
Tangu kuanza kwa ugonjwa wa Ebola kumekuwapo na malalamiko ya watu wanaotoka Barani Afrika kutengwa kwa kutopewa huduma za kijamii nchini Korea  kusini ikiwamo kutoruhusiwa kuingia katika Migahawa na usafiri wa umma kwa madai ya kuwa huenda wana virusi vya Ebola.

Aidha, baadhi yao wamedai watu weusi wanaposimamisha TAXI hazisimami kutokana na hofu ya virusi hivyo vya Ebola.
                                          MWISHO.




No comments:

Post a Comment